AHADI iliyotolewa na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM)
mkoa wa Iringa Jesca Msambatavangu kwa katibu mkuu wa chama hicho Taifa,
Abdulaman Kinana kwamba watakibwaga
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) katika uchaguzi mdogo wa madiwani
mkoani hapa, imekuwa kweli.
Msambatavangu alimueleza Kinana alipopita hivi karibuni mjini
Iringa wakati akielekea mkoani Njombe kwa ziara ya kikazi kwamba CCM itapata
ushindi wa kishindo kwenye uchaguzi huo katika kata ya Ng’ang’ange wilayani Kilolo na Mbalamaziwa, wilayani
Mufindi.
“Niliahidi na imekuwa kweli kwasababu kazi ya maendeleo inayofanywa
na serikali ya CCM inazidi kurejesha imani kwa wananchi na inadhihirisha jinsi
wanavyopuuza kelele za baadhi ya wanasiasa wanaopinga maendeleo yanayofanywa,”
alisema
Akitangaza
matokeo ya uchaguzi huo katika kata ya Ng'ang'ange, msimamizi msaidizi wa
uchaguzi huo, Esabela Kamwela alisema jumla ya wapiga kura
919 kati ya 1087 waliojiandikisha walishiriki uchaguzi huo.
Alisema Chadema
ilimsimamisha Lucas Chahe huku CCM ikimsimamisha Nangamleki Yohanes
katika uchaguzi huo uliomaliza katika hali ya utulivu na amani.
Kamwela alisema katika uchaguzi huo kura 16 ziliharibika
huku mgombea wa Chadema akianguka
vibaya kwa kupata kura 217 na mgombea wa CCM akiibuka kidedea
kwa kuzoa kura 686.
Katika
kata ya Mbalamaziwa ambako Chadema ilijipata matumaini ya ushindi kwa
kile kilichoonekana mikutano yake kupata idadi kubwa ya watu, mgombea wake alibwagwa
vibaya dhidi ya mgombea wa CCM.
Katika
kata ya Mbalamaziwa ambako ni jirani kabisa na kata ya Nyololo ambayo
imeingia katika vitabu vya historia baada Septemba 2, mwaka jana wananchi wake
kuhuhudia tukio ambalo halikuwahi kutokea katika nchi hii la mwandishi wa
habari Daudi Mwangosi kuuawa wakati Chadema ikiendelea na harakati zake za
kuimarisha chama chao, mgombea wake Ezekiel Mlyuka aliambulia
kura 185 tu kati ya kura 1,611 zilizopigwa.
Mgombea wa CCM, Zuberi Nyomolelo aliibuka mshindi wa kiti
hicho cha udiwani baada ya kupata kura 1,426; kura 26 zikiharibika .
Katika
mazingira ya kufurahisha, wagombea wa vyama vyote wameyakubali matokeo hayo,
huku wafuasi wa CCM na wateule wao wakiendelea na shamrashamra wakisubiri siku
ya kuapishwa kwa ajili ya kuwatumikia wananchi.